Home Simulizi Fumbalo – Sehemu Ya Nane

Fumbalo – Sehemu Ya Nane

488
0

Mtunzi: Baraka Oscar

Baruapepe: info@vunjambavu.com

Ilipotimu saa kumi na moja na nusu alfajiri tayari kituo kilikuwa kimaanza kupokea wasafiri ambao walikuwa wanaenda mikoa mbalimbali hususani Dar es Salaam. Siku zote abiria hufika alfajiri na mapema ili kuwahi magari yanayotoka Njombe kwenda Dar es Salaam. Hayo ndiyo yenye uhakika zaidi kwani yale ya Songea au Mbeya wakati fulani hufika yakiwa yamejaa! Zile kelele za baadhi ya abiria zilimwamsha Gadau ambaye naye bila hiyana alilazimika kumwamsha mwenyeji wake Jerome!

“Naona kumekucha ndugu yangu, amka!”
“Usiku mfupi sana.”

Hayo yalikuwa ni mazungumuzo mafupi mara baada ya wote wawili kuamka. Makambako ni mji wenye baridi kali sana hivyo wakati huo wa alfajiri uliambatana na kijiubaridi kikali sana kinachotafuna mpaka mifupa.


Saa moja baadaye, Jerome alimfahamisha Gadau kuwa muda huo ilikuwa ni wakati wa kurejea nyumbani. Ofisi nyingi za kukatisha tiketi zilikuwa zimefunguliwa na kituo cha magari kilikuwa kina watu wengi jambo ambalo lisingehitaji tena ulinzi wake. Iliwachukua dakika kadhaa tu kufika nyumbani kwa Jerome aliyekuwa anaishi mitaa ya Mbeya Road! Jerome alikuwa anaishi kwenye kijijumba cha kupanga cha vyumba viwili! Haikuwa nyumba nzuri na maisha yake yalionyesha alikuwa na shida nyingi tu za maisha.

Baada ya kazi ya ulinzi, Jorome alikuwa anafanya kazi ya kufyatua matofali ya kuchoma na kuyauza ili kujiongezea kipato. Kazi hiyo aliifanya peke yake kila siku. Baada ya mlo wa nguvu walioupata asubuhi yaani ugali kwa samaki wa kukaushwa jamii ya kambale, Jerome alimchukua Gadau mpaka kondeni alikokuwa akifyatua matofali.

“Haya ndiyo maisha yangu ndugu, nataka nifyatue matofali mia tano halafu nitarudi nyumbani saa nane kupumzika ili nijiandae kwenda lindoni”
“Kila siku wafanya hivi?”
“Yaani mimi sina Jumapili wala sikukuu!”
“Uwe unasali bwana hata siku moja moja!”
“Mara moja moja sana huwa naenda kusali Pasaka na Noeli”

Hayo yalikuwa ni baadhi ya mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea baina ya Jerome na Gadau huku wanakanda udongo tayari kwa ajili ya kufyatua matofali. Matofali haya Jarome aliyauza kwa matajiri mbalimbali wa makambako ambao walikuwa wanatafuta matofali ya kujengea nyumba zao.

Biashara hiyo ilimpa umaarufu sana lakini haikuyabadili sana maisha yake kwani Jerome aliendelea kuwa na maisha duni sana siku baada ya siku. Kama kawaida ilipotimu saa nane, walirejea nyumbani kupumzika. Suala la kuoga lilikuwa linafanyika huko huko kondeni ambako kulikuwa na kijito kidogo kinachotiririsha maji msimu mzima!

Gadau alianza kuyaona maisha yake kama filamu au mchezo wa kuigiza! Ilibidi taratibu aanze kuyazoea kwani yeye hakuwa anaenda kulala lindoni kila siku japo siku moja moja alilazimika kwenda kulala na Jerome lindoni! Muda mwingi Gadau alikuwa anashinda kondeni kufyatua matofali na taratibu biashara yao ikaanza kuchanganya kwani uwezo wa kuzalisha matofali kwa siku uliongezeka mara dufu na kwa pamoja walipata morali wa wa kutengeneza matofali mpaka elfu tano kwa siku!

Gadau hakuwa na shughuli nyingine na aliacha kabisa kufanya mazoezi kama ilivyokuwa kawaida yake. Mara kadhaa alikuwa anajichanganya vijiweni maeneo ya ubena kucheza bao na drafti. Siku zilisogea na hakuwa na mkakati wowote wa kurejea Saja. Taratibu alianza kujikusanyia marafiki mbalimbali huko kwenye mizunguko yake.


Siku moja akiwa ametoka maeneo ya ubena alikokuwa anacheza bao na drafti, akiwa katika vichochoro kadha wa kadha vya Makambako alishtuka kapigwa nondo ya kichwa na watu asiowafahamu! Alijitahidi kujikaza akijaribu kupambana lakini maharamia hao walimwongeza nondo nyingine mbili za kichwa zilizompeleka chini na akapoteza fahamu!

Ukanda wa Makambako hadi Mbeya ulikuwa umekumbwa na wimbi la wapiga nondo! Watu hawa walikuwa wanawavizia watu wanaochelewa kurudi majumbani kwao nyakati za usiku na kuwapiga nondo za vichwani! Hii ilitokana na kile kinachoaminika kuwa ni imani za kishirikina. Kwa mujibu wa wenyeji, nondo hizo zilitumika kutundikia nyama mabuchani ili nyama iuzike!

Hii ni moja ya imani za kutisha zaidi katika maeneo haya ya Makambako. Ili nondo ifae ilitakiwa ipakwe damu ya mhanga anayepigwa na hiyo nondo. Mpaka wakati huo Makambako pekee ilikuwa imepatwa na wahanga kumi na saba ambao walipigwa na nondo. Kati yao kumi na moja walifariki duni na sita pekee ndiyo walionusurika na mauti. Gadau alikuwa ni mhanga wa kumi na nane kupigwa nondo ya kichwa na watu ambao hawakufahamika mtandao wao. Hakika mbuzi wa masikini hazai!


Wakazi wa Makambako walikuwa wanaogopa sana kutembea nyakati za usiku na ilikuwa kawaida ikifika saa kumi na mbili jioni utaona watu wanakimbia makwao kujifungia. Hali hii ilipafanya Makambako kuwa pahala pasipo salama lakini hakuna hatua za dharura zilizochukuliwa na serikali kudhibiti uharifu huo kitendo kilichopelekea watu takribani kumi na nane kushambuliwa kwa mashambulizi yanayofanana, yaani ya kutumia nondo!

Itaendelea……

**********

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here