Sijui Nani Katuroga
Leo ngoja niseme, huwa nashangaa sana na sijui nani katuroga. Imesambaa video moja ambayo inamhusu mwanamke mmoja ambaye anatajwa kuwa msukule. Kuna mengi sana yameelezwa kulingana na tukio halisi. Nami nitakuonyesha video hiyo papa hapa!
Tatizo langu si kile ambacho kinaelezwa na wengi kuwa mwanamke yule ni msukule lahasha. Tatizo langu ni vile ambavyo watu wa namna hii wanavyohudumiwa. Ushirikiana kama unauamini shauri yako, lakini hakuna jambo ambalo linaniumiza na tumekuwa hatujifunzi pale anapokutwa mtu katika hali kama ya mwanamke huyo halafu akaonekana kituko!
Matarajio yangu nilitegemea gari lakubebea wagonjwa wa dharura lingeitwa na kabla ya kuulizwa upuuzi wowote ule, yule mwanamke angepelekwa hospitali. Matokeo yake anapakiwa kwenye Carry tena kwa kughalaghazwa nyuma pasipo na boksi au godoro la kumpunguzia mtikisiko. Mbaya zaidi hata nguo tu ya kumfunika hapewi.
Ila watu wanaweza kupiga picha na video na kuzisambaza kwenye mitandao kama vile wanamsaidia. Kwa hali aliyonayo wala huhitaji kuhoji kama anahitaji kupelekwa hospitali liwe ni ndilo tukio la awali na badala ya watu kuandaa huduma ya kwanza inayomfaa mtu anakuja na swali kama hili, “umeolewa?” Sasa kama hajaolewa utamwoa wewe?
Ifike wakati tuanze kutambua kuwa kuna mambo ambayo ni ushirikina lakini pia kuna mambo ambayo ni ya kibinadamu tu yanayohitaji kushughulikiwa. Tanzania ni moja ya nchi ambayo watu wengi sana hufariki kwa sababu ya kukosa huduma ya kwanza tu pindi wanapopatwa na madhara ya kiafya.
jamani, hata kama huyu mwanamke ni msukule, alihitaji huduma ya kwanza ya kitabibu kwa haraka zaidi. Maadamu anaonekana kwa macho ya kibinadamu basi alistahili huduma za kitabibu tena kwa staha! Haya sasa, hebu angalia hii video na jaribu kutazama kwa mwono mwingine na si huu ambao wengi wamekuwa wakimtazama mwanamke huyu.
Video Hii Hapa
(Tahadhari, Video Hii Inaweza kuwa na Picha za kuudhi)


