Home Simulizi Fumbalo – Sehemu Ya Tatu

Fumbalo – Sehemu Ya Tatu

466
0
blackmamba
Huyu ndiye nyoka mamba mweusi; nyoka anayeaminika kuwa na sumu kali zaidi Duniani!

Maneno mengi sana yalisemwa kadri siku zilivyokuwa zikizidi kukatika, kila mtu alikuwa anatoa hadithi yake kwa jinsi akili zake zilivyokuwa zinamtuma. Wapo ambao walimlaumu Gadau kwa namna moja au nyingine lakini lawama nyingi zaidi zilielekezwa kwa mzee Majaliwa Kiswaga. Uvumi uliokuwa umetanda kijijini hapa ni kwamba Gadau alikuwa kapoteza maisha baada ya kujeruhiwa na mzee Majaliwa. Hii ilitokana na ukweli kwamba miezi mitatu ilikuwa imepita na hakukuwa na taarifa yoyote ya kuthibitisha uhai au umauti wa Gadau. Hivyo kila mtu alikuwa anatengeneza hadithi yake ili aifariji nafsi yake. Watu wengi sana walikuwa wanampenda Gadau hivyo hakuna aliyetaka kuamini kwamba Gadau anaweza akawa kapoteza uhai wake.

Hali hii ilimkondesha sana mzee Majaliwa maana alianza kutengwa na jamii taratibu. Hakupata fursa ya kujumuika na wazee wenzake kwa sababu ya simanzi la moyo alilopata kutokana na jinsi jamii ilivyolipokea tukio hilo la kumshambulia na kumjeruhi Gadau kitu kilichopelekea kutoweka kwa kijana huyo na kutokomea kusikofahamika.

Ilikuwa ni kawaida likitokea jambo ambalo lilihitaji ushirikiano wa wanakijiji, mbiu ilipigwa na mara zote iliposikika mbui au kengele ya kijiji, wanakijiji walikusanyika na silaha kuashiria uwepo wa tukio lililokuwa linahitaji ushirikiano.

Aidha Gadau alipigiwa mbiu kwa muda wa majuma mawili mfululizo kila siku na wanakijiji walikuwa wakitembea kwenye mapori kumsaka Gadau wakiamini kama umauti ulimfika basi watauona mwili wake jambo ambalo halikufanikiwa kabisa. Kwa bahati mbaya zaidi tukio hilo la kumtafuta Gadau lilileta majonzi zaidi katika kijiji kitendo kilichopelekea mwenyekiti wa kijiji kuamuru zoezi lisitishwe!

Ilikuwa ni siku ya kumi na nne, Alhamisi; tangu kutoweka kwa Gadau, kundi mojawapo la vijana waliokuwa wanamtafuta Gadau likikabili mapori na vichaka vya uelekeo wa kijiji cha Itengelo, lilipatwa na dhoruba pale mmoja wa vijana hao alipoumwana na nyoka mamba mweusi. Jamii hii ya nyoka ndio inayoaminika kuwa na sumu kali inayosambaa haraka sana mwili kuliko nyoka wengine wowote wanaopatikana ukanda huu wa Saja na duniani pia. Vijana wenzake walifanya juhudi ya kumkimbiza Magembe kijijini ili apate tiba.

Kupambana na aina hii ya nyoka si jambo dogo kwani nyoka huyu ana uwezo mkubwa wa kuuma watu au ng’ombe hata ishirini kutokana na sifa yake kubwa ya kutokubakiza meno anapouma. Pia inasemekana nyoka huyu akikuuma hutumia nguvu nyingi sana kuisukuma sumu yake kitendo ambacho humfanya apoteze fahamu kwa takribani dakika moja mpaka tatu na mara zote inaaminika, nyoka mamba mweusi huuawa kirahisi mara baada ya kuuma kitu. Hiki ndicho kilichokea, kwani mara baada ya Magembe kung’atwa, yule nyoka alijipigiza chini akatulia kimya kwa dakika kadhaa. Wakati huo Magembe alikuwa anaugulia paja lake la mguu wa kushoto kutokana na maumivu makali aliyoyapata baada ya kuumwa na nyoka huyo. Kitendo kile kiliwapa nafasi wale vijana wenzake kumshambulia nyoka yule kwa mawe na kufanikiwa kumwua ndipo walipoanza safari ya kurudi na majeruhi wao pamoja na nyoka mkubwa aliyekuwa kamwuma Magembe.

Kabla ya kumbeba Magembe, Lusajo; mmoja wa vijana waliokuwa kwenye kundi la kumsaka Gadau alichana shati lake na kutoa upinde wa shati lake na kulifunga paja la Magembe ili kupunguza kasi ya sumu isisambae kwa uharaka zaidi. Ilisukwa machela ya kamba za miombo na majani haraha haraka ili waweze kumbeba Magembe kwa urahisi zaidi. Dakika kumi zilitosha kabisa kusuka machela ya kamba na majani laini ambayo ni maarufu sana kwa kuezekea nyumba.

Wakiwa wamekwisha tembea kwa takribani dakika hamsini na tano walianza kusikia Magembe akikoroma na kupumua kwa nguvu sana. Haikuwa ni dalili nzuri kwani muda mfupi baadae walianza kuhisi harufu ya kinyesi. Lusajo alishauri,

“jamani nafikiri mnasikia hiyo harufu, inawezekana kajisaidia tumweke chini ili tumwangalie.“Sawa”,

mmoja wa vijana waliokuwa wamembeba Magembe alijibu kuashiria kuiafiki kauli ya Lusajo. Waliamua kumshusha chini majeruhi ili waone ni kitu gani kilikuwa kinaendelea. Hali ya Magembe ilikuwa ni mbaya sana na alikuwa kalegea mwili wote huku haja zote zikimtoka bila kizuizi.

“Obadia.”

“Naam!”

“Kimbia nyumbani ukamtafute mzee Mwenda uje naye huku umwelieze klichotokea aje Na dawa ili tuokoe maisha ya ndugu yetu hapa, jitahidi kukimbia uwezavyo na sisi tunakuja taratibu kupitia njia ya darajani”,

Lusajo alimwagiza Obadia mmoja wa vijana waliokuwepo kwenye kundi hilo, ila hiana wala kuhoji, Obadia alitimua mbio kuelekea kijijini kumfuata mzee Mwenda. Mzee huyu alikuwa ni maarufu kwa tiba za asili katika kijiji cha Saja.

 

Hali ile iliwashtusha wengi na baadhi ya rafiki zake walianza kulia wakiamini roho ya Magembe ilikuwa inaelekea kuuacha mwili wake kitambo kidogo. Uvumilivu uliwashinda na wakajikuta wakiangua vilio vya uchungu mkuu!

“Kheee! Nyamazeni, hamjui ni vibaya kumlilia mgonjwa?”,

Lusajo aliwafokea wenzake waliokuwa wameshindwa kujizuia na kuanza kuangua vilio mapema walipoona mwelekeo wa Magembe kupona ulikuwa ni hafifu sana. Lusajo alionyesha ujasiri mkubwa sana huku akijaribu kila namna ya kumsaidia rafiki yake lakini nafsi yake haikusita kumsuta kwa kile alichokuwa anakiona.

Ghafla Lusajo alipata wazo,

“Naomba mwondoke kwa dakika kumi nahitaji kubakia na Magembe”

 Kauli hiyo kila mtu aliitii kwani kwa kile alichokuwa amekifanya Lusajo kilitosha kumfanya awe kiongozi wao pasipo pingamizi. Baada ya wenzake kusogea umbali wa kama mita thelathini, Lusajo alimwita Magembe na kwa sauti ya chini sana, Magembe aliitika.

“Rafiki yangu, unaamini kwamba kuna MUNGU?”

Lusajo alimhoji kwa upole rafiki yake.

“Ndii…oo”

 “Naomba unifatishe maneno haya, MUNGU wangu.”

“MUNGU wangu.”

 “Wewe ndiwe utupaye uhai na kutupatiliza mauti.”

“Wewe ndiwe utupaye uhai na kutupatiliza mauti.”

 “Wajua mianzo yetu na miisho yetu.”

“Wajua mianzo yetu na miisho yetu.”

”Tazama sasa hali yangu, naja kwako unisamehe uovu wangu wote”

 ”Tazama sasa hali yangu, naja kwako unisamehe uovu wangu wote.”

 “Nipatie nguvu na ujasiri.”

 “Nipatie nguvu na ujasiri.”

 “Na ikiwa ni mapenzi yako huu uwe ndio mwisho wa safari yangu ya hapa duniani, nirehemu niurithi Ufalme wako.”

“Na ikiwa ni mapenzi yako huu uwe ndio mwisho wa safari yangu ya hapa duniani, nirehemu niurithi Ufalme wako.”

 “Hili ndilo ombi langu kwako, na mapenzi yako yatimizwe.”

 “Hili ndilo ombi langu kwako, na mapenzi yako yatimizwe.”

 “Amen!”

 “Amen!”

 

Tukio hili lilipomalizika, hali ya Magembe ilizidi kubadilika na kuwa mbaya zaidi. Macho yake yalianz akuwa ya rangi ya kahawia na alianza kutokwa na udenda mdomoni mwake. Hali hii ilimpa hofu sana Lusajo na akazidi kumpa moyo rafiki yake,

“jikaze rafiki yangu, tunakutafutia dawa haraka iwezekanavyo, Endelea kupigania uhai wako rafiki.”

“Nisamehe, Ni..samehee!”

“Nani akusamehe Magembe?”

“Naona watu wazuri, naona nchi nzuri!”

 

Baada ya mazungumzo hayo, Magembe alikata kauli na akaanza kukoroma kwa sauti ya kutisha kidogo. Lusajo aliwaita wenzake ili wamsaidie kumbeba Magambe. Kwa mwendo wa kasi, safari ya kumrejesha Magembe kijijini ilianza tena. Lusajo alionekana ni mwenye huzuni sana na safari hii hakuzungumza jambo lolote.  Takribani saa mbili na nusu baadaye, kundi la vijana wapatao ishirini lilimfikisha Magembe katika zahanati ya kijiji. Muuguzi wa zamu alimpokea lakini baada ya uchunguzi wa awali, muuguzi aligundua kuwa magembe alikuwa kafariki dunia.

“Nesi, tusaidie Magembe kaumwa na nyoka”

Lusajo alimhimiza muuguzi awasaidie kumpa tiba ya haraka Magembe mara tu walipomfikisha zahanati. Bila hiana muuguzi wa zamu, Amida Mbanga alimpokea Magembe.

“Mlazeni kwenye hiki kitanda”

Amida aliwaamuru Lusajo na marafiki zake wamlaze Magembe kitandani na baada ya hapo alihoji,

“Ni nyoka wa aina gani kamuuma?”

“Pingang’ombe!”

nyoka mbamba
Nyoka Mamba Mweusi

 

Pingang’ombe ni jina maarufu sana liliokuwa linatumika kumtambulisha nyoka mamba mweusi katika ukanda huu. Jina hili la nyoka mamba mweusi halikuwa linafahamika sana miongoni mwa wakazi wa kijiji cha Saja. Alipewa jina hili kwa sababu nyoka huyu alikuwa anauwezo wa kuwauma hata ng’ombe ishirini na kuwaua wote kwa muda mufipi sana kutokana na sumu yake kali nyenye kasi. Pia pingang’ombe anauwezo wa kusimamia mkia na inasemekana kuwa mara nyingi nyoka huyu amekuwa akiuma watu utosini au mbavuni kutokana na namna yake ya kuuma ambayo ni lazima aruke!

“Nini?”

“Ndiyo nesi, kaumwa na pingang’ombe”

“Mmejuaje?”

“Tumemwua”

“Yuko wapi?”

 

            Amida alipigwa butwaa alipoona Munubi akimwaga sakafuni joka kubwa sana lililokuwa limemwuma Magambe. Kitendo kile kilimshtua sana Amida akataka kukimbilia nje,

“Mtoeni nje, mmoja wenu abaki wengine subirini nje”

Malumbo alimchukua yule nyoka na akafuatana na vijana wenzake huku wakiwaacha Lusajo na Amida. Lusajo alibakia na muuguzi katika chumba cha tabibu ili aweze kumsaidia jambo lolote ambalo lingehitaji usaidizi katika kufanikisha huduma kwa Magembe.

 

Amida alilazimika kufanya uchunguzi wa awali kabla ya kumpa dawa mgonjwa! Hii ilikuwa ni pamoja na kupima mapigo ya moyo na pumzi. Ukweli ni kwamba Magembe alikuwa hapumui lakini kila mtu alidanganywa na macho yake yaliyoonyesha kalala usingizi mzito. Katika uchunguzi wake wa awali kabisa, Amida aligundua kuwa Magembe alikuwa kafariki dunia muda mrefu. Mwili wake ulikuwa umepoa na alikuwa kama mtu aliyelala usingizi na kuyafumba macho yake kwa upole. Amida alimwangalia usoni Lusajao ila akashindwa namna ya kumweleza kile alichokibaini.

“Niambie, usinifiche kitu napenda kujua kama kilichotokea ni kile nachokihisi!”

“Unahisi nini?”

Amida alihoji kwa upole huku akitumia toni ya chini sana na macho akiyatumbua kumwangalia Lusajo.

Hali hii iliashiria kuharibika kwa mambo kitu kilichomfanya Lusajo kuondoka bila kuaga. Halikuwa ni jambo rahisi sana kusadiki kwamba Magembe alikuwa kafikwa na umauti lakini hilo ndilo lililokuwa limetokea.

Kuna wakati Lusajo alidhani labda ule muda waliotumia kumwua yule nyoka aliyekuwa na urefu wa futi kumi na kumi na mbili ndio uliosababisha wakapoteza muda mwingi. Lahasha, ukweli ni kwamba, nyoka huyu akikuuma unatakiwa kupata tiba mapema zaidi yaani ndani ya dakika kumi za awali!

Iteendelea…………..


 

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here