Home Simulizi Fumbalo – Sehemu Ya Saba

Fumbalo – Sehemu Ya Saba

445
0

Mtunzi: Baraka Oscar

Barua pepe: info@vunjambavu.com

Wiki moja baadae, Gadau aliruhusiwa kutoka hospitali lakini alikuwa chini ya uangalizi wa polisi. Polisi walipewa taarifa kwamba Gadau alikuwa kapona na alitakiwa kuruhusiwa kutoka hospitali. Afisa mmoja wa upelelezi alitumwa kwenda kumfuata Gadau na kumrudisha kituo cha polisi cha Makambako kwa ajili ya mahojiano zaidi.

Baada ya uchunguzi wa kina na mahojiano ya muda mrefu kidogo Gadau aliachiwa huru na maelezo yake yalitosha kumwepusha na sekeseke la “kunyea ndoo!”

Gadau aliingia kwenye mitaa ya Makambako akiwa hana mwenyeji wala ndugu wa kufikia. Hakuwa mgeni sana katika mji wa Makambako ila alikuwa hana ndugu au jamaa wa karibu ambaye angeweza kwenda kwake. Suala la kurudi Saja lilikuwa haligongi kabisa kwenye kichwa cha Gadau kwani kila alipokumbuka ule mkasa wa kukatwa na mundu tukio lililofanywa na ‘baba mkwe wake’ alikuwa anajisikia vibaya sana!

Taratibu Gadau alijisogeza katika kituo cha mabasi cha Makambako ambako aliamini angeweza kupata jambo la kufanya. Wanasema mtembea bure si mkaa bure huenda akaokota! Kituo kilikuwa kina pilika nyingi, abiria waliingia na kutoka maana Makambako ni mji wa kibiashara hivyo watu wengi huingia na kutoka kila siku.

Hatimaye jua lilianza kutoweka katika uso wa dunia na Gadau alikuwa hajatia kitu chochote tumboni. Pia alikuwa hajui giza likiingia angelaza wapi mbavu zake. Mtima wake ulianza kuingiwa na wasiwasi na ilipotimu saa kumi na mbili za jioni watu walianza kupukutika kwa kasi sana wakielekea majumbwani mwao.

Gadau alijikuta akiwa peke yake na baadhi ya watu kama wawili watatu ambao dhahiri walionekana ni walinzi wa baadhi ya maduka na vibanda vilivyopo kituoni hapo. Uzalendo ukamshinda Gadau akaanzisha mazungumuzo na mmoja wa walinzi waliokuwa wanalinda duka la tajiri mmoja wa Makambako maarufu kama Mchape!


Mchape alikuwa na magari kadha wa kadha yaliyokuwa  yakifanya safari za Songea, Iringa, Mbeya, Ilembula na Ubaruku.

“Kamwene.”

Gadau alimsabahi yule mlinzi na kuanzisha mazungumzo.

“Kamwene.”

Yule mlinzi alimjibu bila hiana.

“Naitwa Gadau, natokea Saja, Wewe ni nani mwenzangu?”

“Alaaaaa! Unatokea Saja? Naitwa Jerome Kikula mtoto wa mzee Kikula wa Makondo!”

“Namjua sana yule mzee anafuga ng’ombe wengi sana na ni mkulima mkubwa sana wa karanga na alizeti.”

“Kumbe unamfahamu, yule ni baba yangu!”

“Kulikoni upo huku na mzee ana ng’ombe na mashamba makubwa?”

“Maisha tu ndugu yangu, nimekuja kujaribu bahati huku mjini lakini kazi yenyewe niliyoambulia ndiyo hii!”

“Kwa nini usirudi nyumbani?”

Gadau alionekana kuendelea kumdadisi Jerome.

“Nitaanzia wapi!”

“Kwa nini?”

“Baba alinikataza sana kuja mjini lakini nikang’ang’ania na nilimwomba anipe laki mbili ili nije mjini. Baba aliuza ng’ombe watatu nikapata hiyo pesa ya kuja mjini kufanya biashara.”

“Duh! Pole sana ndugu yangu!”

“Hapa nilipo sina nyuma wala mbele na maisha yamegoma kabisa, kurudi nyumbani naona aibu sijui hata nitaanzaje.”

Maongezi yalionyesha kukolea, hakika kila mmoja alikuwa anahitaji faraja. Baada ya maelezo hayo Jerome alipenyeza swali,

“Na wewe mwenzangu kulikoni?”

Jerome akahoji huku akiachia tabasamu lenye shauku ya kutaka kujua kilichomsibu Gadau. Gadau hakuwa na namna nyingine zaidi ya kumsimulia mkasa mzima uliokuwa umemsibu. Jerome alimwonea huruma sana Gadau na wakashauriana kwa kina namna ya kukabiliana na matatizo yao.

Kwa muda mfupi sana wakawa wamezoeana na kuzungumuza mambo mengi. Siku hiyo Gadau alilalia karanga mbichi za kuchemsha ambazo Jerome alikuja nazo akizitafuna kutoka kwake. Njaa ilikuwa inamwuma sana lakini hakuwa na namna. Jerome alimsihi avumilie kwani kesho yake wangeenda kula kwake walau ugali kwa kambale wa kukaushwa.

Kwa kweli kazi ya ulinzi ni ngumu, si jambo jepesi kukaa macho usiku kucha hivyo Jerome alitandika kijimkeka chake ambacho alikuwa anakitumia kila siku kujilaza kwenye kivaranda cha duka alilokuwa analilinda. Siku hiyo alipata mtu wa kukesha naye lakini ilipofika milango ya saa nane usiku wote wawili wakapitiwa na usingizi!

Itaendelea …………


LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here