Sehemu Ya Pili
Mtunzi: Baraka Oscar
info@vunjambavu.com
Kama kawaida yake, Gadau alipiga jaramba kwa kuzunguka uwanja mara tano kwa kasi kabla ya kujumuika na wachezaji wenzake kwa ajili ya mazoezi ya pamoja. Timu ya Saja ilikuwa inatisha kwa kucheza mpira wa kasi na pasi fupi za uhakika. Katika kata ya Saja ni timu moja tu ya kijiji cha Ikulimambo ndiyo ilikuwa inaonyesha upinzani mkali zaidi. Wachezaji wa Saja walilazimika kutumia nguvu ya ziada kuishinda timu hiyo kila mara walipokuwa wakikutana katika kombe la kugombea Ng’ombe lililokuwa linadhaminiwa na tajiri mmoja maarufu kwa jina la Mjengwa! Mshindi alikuwa ananyakua kitita cha shilingi laki moja na ng’ombe mzima!
Mashindano haya yalikuwa yanavutia watu wengi na yalikuwa yanafanyika mara mbili kwa mwaka. Mpaka sasa michuano hiyo ilikuwa imefanyika mara saba katika kipindi cha miaka minne na michuano iliyokuwa inafuatia ilikuwa ni mara ya nane katika kipindi cha miaka minne. Mara tano timu ya kijiji cha Saja ilinyakua ubingnwa na mara mbili kombe hilo lilinyakuliwa na kijiji cha Ikulimambo. Hivyo vijiji vingine viliendelea kuwa wasindikizaji maana mara zote hizo ni Saja na Ikulimambo tu ndio timu pekee zilizokuwa zinakutana fainali.
Ilikuwa si jambo rahisi kuisifia timu ya Saja pasipo kumsifia kocha wa timu hiyo Mzee Mugumba. Mzee huyu alijozolea umaarufu mkubwa kwa kukinoa kikosi cha timu ya kijiji. Aidha hakuwa amesomea ualimu wa mpira wa miguu isipokuwa alipata ujuzi huu alipokuwa akifanya kazi na kampuni ya Kajima huko Chimala, Mbeya miaka kumi na mitano iliyopita. Hivyo ujuzi mdogo alioupata huko akiwa kama mlinda mlango wa timu ya Kajima, aliuleta katika kijiji chake mara baada ya kuacha kazi. Hivyo hakuna aliyekuwa anatilia shaka uwezo wake na Mzee Mugumba alikuwa anaweza sana kuijenga timu ikacheza kutafuta ushindi.
Giza lilipoanza kuimeza nchi, mazoezi yaliahirishwa na baada ya mawaidha ya mwalimu; wachezaji na baadhi ya wapenzi wachache wa soka walianza kurejea makwao kujipumzisha. Huu ndio usiku ulioyabadili kabisa maisha ya Gadau. Gadau alijikongoja taratibu kuelekea nyumbani kwake. Alipofika nyumbani ghafla alishtushwa na uwepo wa Mzee Majaliwa Kiswaga na mara mapigo yake ya moyo yalianza kumwenda mbio.
“Wewe shetani wa mguu mmoja uliyekosa haya unajifanya kidume cha mbegu hapa kijijini mpaka umeniharibia mwanangu, sio ehee?”,
mzee Kiswaga aling’aka kwa sauti iliyoonyesha hasira isiyo ya kadri.
“Nitauweka wapi uso wangu katika kijiji hiki? Nakuuliza wewe mbwa koko husikii?”
Gadau alikuwa amezubaa kwa mshtuko na hakuamini kile alichokuwa anakisikia. Wakati uo huo, mzee Kiswaga alikuwa anamkaribia na kutokana na kiza kuanza kuingia, Gadau hakuona kama mzee Kiswaga alikuwa ameshika mundu!
“Mamaaaaa nakufaaaaa”,
alisikika Gadau akiugulia maumivu makali kwa sauti ya juu baada ya mundu kuparaza bega lake na kumfunua nyama ya mkono wake. Gadau alianza kuvuja damu sana katika mkono wake wa kushoto kutokana na ukweli kwamba ule mundu ulikata moja ya mishipa mikubwa ya damu.
“Baba utamwua mtoto wa watu, naomba umsamehe, nipo chini ya miguu yako baba yangu” “Kelele na wewe malaya usiyejua kuchagua, umekosa wanaume wote hawa hapa kijijini ukaja kulala na mvuvi haramu huyu?”,
Mzee Kiswaga alimziba mdomo binti yake Dafrosa. Dafrosa alikuwa ni mtoto pekee wa mzee Majaliwa Kiswaga aliyempata baada ya kumwoa Jobiso Mwinamila, binti wa aliyekuwa chifu wa Kijiji cha Saja, Chifu Mwinamila.
Kitendo kile kilimtisha sana Gadau, aliingiwa na hofu sana pale alipobaini damu inamwagika kama maji ya bomba. Alijitahidi kufunga mkono wake na shati alilokuwa amelivaa ili kuzuia damu isimtoke kwa wingi huku anakimbia maana mzee Kiswaga alikuwa bado anamfukuza huku kashika mundu. Gadau alimshinda mbio mzee Kiswaga na kufanikiwa kutokomea gizani. Akili ya Gadau ilishindwa kabisa kufikiri na hakujua aelekee wapi kwa wakati huo na alijikuta anafuata barabara iendayo Makambako. Makambako ni mji mdogo ulio umbali wa saa tano kwa kutembea, Gadau hakuona umbali huo na akajikuta akiamua kuelekea Makambako. Alitembea usiku kwa takribani saa tano ndipo alipogundua kwamba amefika mbali sana. Mwili wake ulikuwa umedhohofika sana na alikuwa kaishiwa nguvu hii ni kutokana na damu nyingi iliyokuwa imemtoka. Ghafla alianza kusikia kizunguzungu na akaanguka chini akapoteza fahamu.
Ilikuwa ni usiku mwingi yapata saa sita na nusu na hakukuwa na msaada wowote ambao angeutarajia kwa usiku huo. Baridi kali ya mji huo wa Makambako ilimzindua takribani milango ya saa nane na nusu usiku ndipo alipogundua alikuwa amelala pembezoni mwa sakafu ngumu sana na hakuweza kubaini au kukumbuka ni mahali gani alikuwa kalala! Kila alipojaribu kunyanyua mwili wake hakufanikiwa na macho yake yalianza kuishiwa nguvu pia akawa anashindwa kuyafungua. Hakika Gadau hakuweza kupata nguvu ya kujinyanyua pale chini hivyo alilazimika kujilaza kabisa.
Mungu si Athumani, dakika chache baadaye lilipita gari la polisi lililokuwa limetokea doria maeneo ya Idofi. Gari hilo lilipofika maeneo ya Makambako jeshini, kwa bahati nzuri kila askari aliyekuwa kwenye gari alimwona Gadau akiwa kalala pembezoni mwa barabara na kwa haraka haraka wote walijua anaweza akawa amegongwa na gari maana Gadau alikuwa kalala kwenye kingo za barabara kuu itokayo Makambako kuelekea Dar es Salaam.
Dereva wa lile gari alisimamisha gari pembeni kisha askari wote kumi na tano waliokuwemo ndani ya gari waliteremka wakausogelea ule mwili uliokuwa umejilaza kandokando ya barabara. Mmoja wao aliamru Gadau ageuzwe kwa sababu alikuwa kalala kifudifudi.
“Afande, hili rijamaa limevuja sana damu sijui limekabwa na wapiga nondo”,
mmoja wa askari alitoa maelezo hayo mara baada ya kumgeuza Gadau.
“Kwani bado linapumua?”. “Ndiyo, afande bado linapumua”.
“Lipakieni kwenye gari twende nalo Ilembula”,
yule askari aliyeonekana kutoa maagizo kwa wengine tangu awali aliwaamuru askari wengine wambebe Gadau na kumpakia kwenye gari.
Msafara wa gari la polisi uliondoka Idofi karibu na kambi ya Jeshi ya Makambako, eneo la tukio na kuelekea Ilembula kwa kasi sana. Wakati huo Gadau alikuwa kapoteza uwezo wake hata wa kuongea na alibakia akitikisa vidole vya miguu na mikono na wakati mwingine alikuwa anashtuka na kujitikisa mwili mzima huku akijarbu kujigeuza bila mafanikio. Baada ya dakika kama ishirini hivi lile gari la polisi lilikuwa linaingia malango ya hospitali ya Ilembula. Gadau alipokelewa na Tabibu na wauguzi wa zamu kwa uangalizi wa hali ya juu kwa vile alikuwa kaletwa na polisi! Mkuu wa kikosi alitoa maelezo mafupi jinsi walivyompata Gadau na baada ya uchunguzi wa awali kufanyika, matabibu walibaini amepungukiwa damu kwa kiwango kikubwa sana na walilazimika kumwongezea damu haraka sana. Yule mkuu wa msafara wa polisi aliwaahidi matabibu kuwa watakuja kumhoji Gadau iwapo atapata nafuu siku mbili baadae.
Matabibu walitumia kila aina ya utaalamu wao kunusuru maisha ya Gadau. Gadau alipelekwa chumba cha wagonjwa mahututi na alifanyiwa vipimo vya damu usiku ule ule kitu ambacho ni nadra sana kufanyika. Baada ya vipimo kukamilika alibainika kuwa alikuwa ni kundi A chanya la damu hivyo alianza kuongezewa damu mara moja.
Ilipotimu saa saba mchana, siku iliyofuta Gadau alizinduka toka katika usingizi mzito nusu mauti. Kwa hali aliyokuwa nayo haikuwa rahisi sana kuamini kama angeweza kurudia uhai wake tena uliokuwa mashakani. Kilichomshtua zaidi ni pale alipojikuta yupo katika chumba asichokifahamu na ghafla akaingiwa na hofu na kupaza sauti huku ikiuliza yuko wapi. Alipotaka kuinuka akagundua kuwa mkono wake wa kuume ulikuwa umefungwa pingu kitandania hivyo asingeweza kuondoka kitandani.
“Nifungueni, nataka kwenda nyumbani”,
Gadau alipayuka. Muuguzi wa zamu alikuwa kasikia kelele za Gadau hivyo aliingia na kumchoma sindano ya usingizi, Gadau akalala fofofo!
**********
Itaendelea Kesho Kutwa Jumapili……….
