Kijiji kilipooza sana mara baada ya vuguvugu hili kuanza kusambaa na hakika lilisambaa kwa kasi sana. Kengele ya kanisa la Kiinjili la Kilutheri usharika wa Saja ilipigwa ikiwa ni kawaida ya kupashana habari za misiba inayowakumba wakristo. Wakristo wengi walikuwa ni wa dhehebu la kilutheri hivyo kulikuwa na kanisa moja kubwa la Kilutheri kijijini. Iwapo ikitokea kafariki muislam, kengele ya kijiji iligongwa kwa mtindo ule ule unaofanana na mtindo wa kengele ya kanisa. Mara zote kengele hizi ziligongwa mara tano na kusitishwa kwa sekunde sitini. Hivyo wanakijiji walishazoea, ilikuwa wakisikia aina hiyo ya mlio wa kengele ya kanisa au ya kijiji ilikuwa ni taarifa tosha kwamba kuna msiba. Kwa ishara hiyo wanakijiji wasio na taarifa hulazimika kujongea mpaka kanisani au kwenye ofisi ya kijiji ili kujua ni nani kapoteza uhai wake na mara zote kulikuwa kunabandikwa matangazo ya kueleza ni nani kafariki na mazishi yatafanyika lini na wapi.
Kijiji kilikuwa kimepwaya kwani hakukuwa na watu wengi kutokana na ukweli kwamba wanaume wengi walikuwa wametawanyika maporini kumsaka Gadau. Wanakijiji wengi waliosikia kengele ile walidhani labda Gadau kapatikana akiwa mfu hivyo walilazimika kuja mbio kanisani kujua ni nani alikuwa kafariki. Lusajo ndiye aliyepeleka taarifa hiyo ya msiba kanisani na kengele ikaanza kugongwa. Kutoka kanisani mpaka ofisi ya kijiji kuna umbali mfupi sana takribani mita mia mbili, Lusajo alipotoa taarifa kanisani alielekea ofisi ya kijiji ili nako akawapashe habari hiyo ya kuhuzunisha. Akiwa njiani alikutana na Obadia! Obadia alianza kuhoji,
“Kuna nini kimetokea?”
“Ulimpata mzee Mwenda?”
Ilikuwa ni swali juu ya swali!
“Sikumpata, bado hawajarudi na wao walienda kumtafuta Gadau!”
“Nilisahau kabisa hilo jambo.”
“Hujaniambia ni kitu gani kimetokea, Magembe yuko wapi?”
Mazungumzo hayo yalikuwa yanaendelea wakati Obadia akilazimika kugeuka na kuanza kuongozana na Lusajo wakielekea ofisi ya mtendaji wa kijiji. Obadia alizidi kupatwa na wasiwasi lakini cha kushangaza Lusajo alikuwa mtulivu wala hakuonyesha kuwa na wasiwasi kwa mwonekano.
“Nakuuliza tena, Magembe yuko wapi?”
“Yupo zahanati!”
“Ina maana hiyo kengele ni yake?”
Lusajo alitikisa kichwa kuashiria kuwa alikuwa anamaanisha ndiyo! Obadia hakuuliza swali jingine zaidi, haraka haraka alitimua mbio kuelekea zahanati ya kijiji. Aliwakuta rafiki zake wamekaa nje ya zahanati wakiwa wamejiinamia kwa huzuni kubwa sana. Kila mtu alikuwa ametahayari na hakika msiba wa Magembe uliwaliza watu wengi sana.
Magembe Bin Lugoya, alikuwa ni mtoto pekee wa kiume wa mzee Masumbuko Lugoya na Bi Atupelie Kiwanga katika familia iliyokuwa ina watoto sita. Watano walikuwa ni mabinti na mmoja alikuwa ni mtoto wa kiume, yaani Magembe. Mzee Lugoya alikuwa ni mtu maarufu sana kwa sababu kubwa mbili; mbali na kufahamika kwa ucheshi wake, mzee huyu aliwahi kuwa mwenyekiti wa chama cha mapinduzi katika kijiji kwa takribani miongo miwili! Alikitumikia chama kwa muda wote huo mpaka alipofikwa na mauti baada ya kupigwa na radi akiwa kilabuni miaka miwili iliyopita.
Hali hii ilizidisha majonzi kwa kwa familia ya Bi Atupelie, mjane aliyepoteza mwanae wa kiume kwa kuumwa na nyoka! Msiba huu unamtokea miaka miwili baada ya kumpoteza mume wake kwa kupigwa na radi kitu kilichopelekea hata sura ya mumewe kutofahamika vema kwani radi lilimwunguza sana. Ilikuwa si jambo jepesi kulipokea na watu walianza kunong’onezana mambo mengi na wengine walianza kufikiri labda ni matukio yenye uhisiano na ushirikina kwa namna moja au nyingine.
“Aaaaha! Umeondoka kama baba yako, bora ungeugua niseme nimeshindwa kukuponyesha baada ya kukuuguza. Mimi Sekiwanga’ nimemkosea nini Mungu mpaka mniache mkiwa namna hii!”
Huku akibubujikwa na machozi ya huzuni, Atupelie aliyasema maneno hayo kwa uchungu sana. Hii ni mara tu baada ya kuwasili zahanati kuushuhudia mwili wa Magembe kutokana na taarifa alizokuwa kafikishiwa kuhusiana na kifo cha mwanae,
“Uwiiii…! Nionyesheni mwanangu! Nataka kumwona mwanangu….”
Amida alimpeleka Bi Atupelie akiwa ameongozana na mabinti zake watano na baadhi ya majirani katika chumba alichokuwa amewekwa Magembe mara baada ya kufariki.
“Ohoooo! Mwanangu, uliniambia asubuhi nikupikie ugali na majani ya kunde ili ukamtafute rafiki yako Gadau ukiwa umeshiba kumbe ndio nilikuwa nakupikia kwa mara ya mwisho! Kwa nini hukuniambia kwamba hutarudi mwanangu! Nitakuwa mgeni wa nani mimi kijiji hiki”
Maneno haya yalimliza kila mtu aliyeyasikia na kitendo hiki kilitokea mara tu baada ya Bi Atupelie kumwona mwanae akiwa kalazwa kitandani kama mtu aliyesinzia huku akitaka kuachia tabasamu laini. Kama mtu angemwangalia Magembe pasipo kufahamishwa kilichotokea ni dhahiri angedhani kalala usingizi tu kumbe alikuwa kafariki dunia!
Itaendelea………….
**********
