Home Simulizi FUMBALO – Sehemu Ya Sita

FUMBALO – Sehemu Ya Sita

438
0

Mtunzi: Baraka Oscar info@vunjambavu.com

Kitendo hicho kilimtenga zaidi na jamii yake kwani alijikuta anajinyanyapaa na kunyanyapaliwa pia na wanakijiji wenzake. Baada ya mkutano taarifa zilimfikia kwamba alikuwa anatakiwa kuhudhuria kikao cha kamati ya nidhamu ya kijiji siku ya ijumaa.

             Hata hivyo, kulikuwa na mgawanyiko wa kimawazo baina ya wanakijiji. Wapo ambao waliamini kuwa Gadau alikosea na yaliyotokea ni kwa sababu ya upuuzi wake. Ilikuwa ni fedheha kubwa sana kwa binti wa kijiji cha Saja kupata ujauzito akiwa anaishi na wazazi wake. Jambo hili lilikuwa linaipa aibu kubwa sana familia kila lilipotokea. Na kwa kumbukumbu za awali, ni mabinti wawili ndiyo waliwahi kupata mimba wakiwa kwa wazazi wao. Mmoja alijiua alipogundua ana mimba, huyu alikuwa ni binti wa mzee Mpiluka.

             Siyawezi Mpiluka alivuta sana hisia za wengi pale alipokutwa kajinyonga karibu na njia iendayo kisimani. Mkasa wake uliwatia simanzi sana wanakijiji na wakalazimika kumtafuta kwa udi na uvumba mwanaume aliyekuwa kampa mimba binti huyo. Nia yao ilikuwa ni kumwadhibu kwa kumzika mzima na marehemu.


Ikumbukwe kwamba katika kijiji cha Saja ilikuwa ni aibu isiyo ya kifani iwapo mtoto wa kike ambaye hajaolewa kupata mimba. Ilikuwa ni ishara mbaya na waliamini familia hiyo lazima iandamwe na mikosi. Kwa bahati nzuri Lukelo Njogopa ndiye aliyempa ujauzito Siayawezi na alifanikiwa kutoroka na mpaka leo haifahamiki yuko wapi!

             Tukio hili ndilo lililomfanya mzee Mgurunde asimfokee wala kumfukuza binti yake Remija kutokana na ujauzito aliopewa na Komesho kijana wa mzee Kidege, mhunzi maarufu kijijini. Licha ya kuwepo kwa fedheha kubwa katika familia, mzee Mgurunde alitumia busara na kunusuru hali ya mwanae akihofia kumpoteza kabisa iwapo Remija angefuata mtazamo wa Siyawezi.

             Ijumaa saa nne asubuhi kikao cha kamati ya ulinzi na usalama kilianza kujadili ajenda mbalimbali zilizokuwa zimewasilishwa. Ajenda kubwa ilikuwa ni hoja iliyokuwa imetolewa na Lusajo siku ya mkutano wa hadhara wa kijiji.

“Natumai kila mmoja wetu anatambua kwa nini tupo hapa”,

mwenyekiti wa kijiji alianza kuvunja ukimya mara baada ya wajumbe wote kuwa tayari kwa kikao. Lakini mzee Kiswaga alionyesha kutoafahamu kwa kina jambo hilo,

“Mimi sifahamu!”

“Usiwe na shaka utafahamishwa mzee wangu”,

Lutengano alimtoa wasiwasi mzee Kiswaga.

 Lutengano, mwenyekiti wa kamati alivuta pumzi kisha akafungua mjadala mzito wa kujadili hatima ya mzee Kiswaga.

“Mimi napendekeza jambo moja,kwa kuwa ushahidi wote unaonyesha mzee Kiswaga katufikisha hapa, alipe ng’ombe mmoja wa kutoa mikosi kwa familia ya Magembe na ng’ombe tisa kwa mama wa Magembe kama kipoza uchungu!”

 Mvutano ulikuwa mkali sana baina ya wajumbe, wapo walioona adhabu ni kubwa sana na wapo waliotaka mzee Kiswaga atengwe kijijini! Baada ya mjadala mkali hatima ilifikiwa, mapendekezo yalikuwa ni ng’ombe watano na atengwe na kijiji kwa miaka mitano!

 Aidha wakati malumbano ya kimjadala yakipamba moto, Lutengano alimtoa nje mzee Kiswaga huku akimwamuru asubiri mjadala ukamilike halafu aambiwe hukumu yake. Alipopewa hiyo taarifa ya mwafaka wa kikao, mzee Kiswaga akaanguka chini na kuzimia!

Itaendelea…………

**********

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here