Mimi ni msomaji mzuri wa magazeti, na msikilizaji mzuri wa redio, huwa naangalia luninga mara chache sana kama nikibahatika kupita mahala kuna luninga. Sasa wiki hii nimesikia mengi kuhusu hizi ziara za kushtukiza za viongozi wetu, nikaona hili ni jambo zuri tena linafaa kuigwa na sisi wananchi wapenda maendeleo. Nikaona nijipange na mimi nifanye ziara kadhaa za kushtukiza katika sehemu mbalimbali zinazonihusu.
Nikaona nianze na ziara ya kushtukiza pale shuleni kwa huyu mwanangu, maana kila siku anakunywa chai na kuondoka na daftari zake na mie sijawahi kwenda shuleni kwao toka nilipomuandikisha shule mwezi Januari.
Nilifika shuleni na kumuona mwalimu mkuu, ambaye alianza kutetemeka nilipomwambia kuwa nimekuja pale kwa ziara ya kustukiza. Sijui alidhani mimi ni mmoja wa mawaziri wapya, maana nilimuona jasho linamtiririka ghafla.
Akanikaribisha ofisini mwake kulikokuwa na vitabu kila kona, na kuita waalimu wote na kunitambulisha kuwa ni kiongozi nimekuja kwenye ziara ya kushtukiza. Nilipojitambulisha kuwa ni mzazi, waalimu wote nikawaona wanaanza kupumua kwa raha. Nikawaambia kuwa mimi nina mwanafunzi pale na nilikuja ziara ya kushtukiza kujua maendeleo yake.
Baada ya mwalimu mkuu kusaka jina la mwanangu nae akanambia, “Mzee huyu mtoto hajaja shule mwezi wa tatu sasa, tulijaribu kukutafuta ikashindikana, hatujui yu wapi!” Jasho likaanza kunitoka mimi, yule mtoto kila asubuhi nampa nauli anaenda shule, na mara nyingi ananiomba michango kumbe hata shule haji.
Niliondoka bila kuaga presha ikiwa juu. Nikaona niende kwenye genge la mke wangu naye nikamfanyie ziara ya ghafla nimhadithie mambo ya mwanaye. Nilipofika pale nikakuta kuna mdada mwingine anauza genge. Nikamsalimu, na kumuuliza mwenye genge nitampataje? Lakini jibu lake lingeniua kama ningekuwa si mkakamavu, “Mume wake kaja kumchukua na gari wameenda kununua shamba Bagamoyo”.
Nikaondoka nimechanganyikiwa, nikajua hapa dawa yangu moja tu, nayo ni Sabrina, mtoto wa Kinyaturu pale ambapo nikipata maudhi huwa naenda kubembelezwa. Nikatwanga mguu kwa Sabrina nae nikamfanyie ziara ya ghafla ili anipoze moyo. Nilipogonga mlango wa chumba chake akatoka mbaba wa miraba minne, akanisalimia kwa upole, “Salama kaka unasemaje?” Jibu likanitoka “Samahani mie nilimkopesha huyu dada wa chumba hiki vitenge, nilikuja kuuliza kama ameshapata hela yangu” Ziara za kushtukiza zinataka moyo wa chuma jamani!!!




