Sehemu Ya Kwanza
Mtunzi: Baraka Oscar
info@vunjambavu.com
Ni asubuhi njema kabisa bwana Gadau aliamka katika kitanda chake kidogo cha kamba na kutoka ndani ya kibanda chake cha ‘mbavu za mbwa’ kilichoezekwa kwa majani laini ambayo huku kwetu huitwa ‘likuvi’. Sina hakika sana kama nafahamu jina la kiswahili la aina hii ya majani ambayo huota ukanda wa Iringa kwa wingi sana. Baada ya kujisafisha kama kawaida ya kila mwanadamu aliyestaarabika aamkapo asubuhi, ni sharti asafishe kinywa chake na kupakaza walau maji usoni mwake ili kuondoa matongotongo machoni, Gadau alivaa nguo zake za mazoezi. Dakika chache baadae, Gadau alikuwa kaanza kufanya mazoezi ya kukimbia; kila siku asubuhi kabla ya kwenda kwenye shughili zake za kujiingizia kipato ilikuwa ni kawaida yake kupiga jaramba walau mizunguko kumi katika kiwanja cha mpira wa miguu wa shule ya msingi Saja kilichokuwa umbali wa kama mita mia tatu toka nyumbani kwake. Utamaduni huu uliigwa na baadhi ya wanafunzi ambao walikuwa wanawahi sana kuja shuleni na wakimwona Gadau anapasha misuli yake moto waliungana naye. Mara zote alijitahidi kila ilipotimu saa kumi na mbili kamili alikuwa kashakanyaga majani hafifu ya kiwanja cha shule hiyo.
Akiwa na uchovu baada ya kukimbia mizunguko kumi, Gadau alianza kurejea nyumbani kwake kwa mwendo wa kujikongoja kiasi. Hakika siku hiyo alionekana kuzidiwa na ile mizunguko kumi kwani hata hivyo alilazimika kutumia muda mrefu zaidi kumaliza kukimbia kiasi cha dakika arobaini na mbili na sekunde thelathini na saba ikiwa ni zaidi ya dakika kumi na saba ya mwendo kasi wake wa kawaida ambao aliutumia siku zote. Jambo la kwanza lilikukwa ni kujimwagia maji ya vuguvugu kisha akanywa chai na viazi vitamu alivyokuwa kavipika usiku wa jana yake!
Gadau hakuwa na kazi nyingine zaidi ya uvuvi. Uvuvi ni kazi ambayo aliirithi kutoka kwa marehemu baba yake, mzee Tesha aliyefariki miaka kumi na miwili iliyopita. Mzee Tesha alikuwa ni mvuvi hodari sana katika kijiji cha Saja na kuna wakati alijizolea umaarufu mkubwa sana, watu wengi walinunua samaki kwake na kuwauza vijiji vya jirani.
“Mwanangu, mimi sikusoma wala sikupata bahati ya kukanyaga darasani.”
Tesha liongea kwa kituo,
“hawa samaki naowauza usiku kucha nashinda bwawani ninataka usome kwa bidii uje unisaidie mimi baba yako.”
Ni ujumbe ambao mzee Tesha alikuwa akimfikishia mwanae siku moja walipokuwa wakitembeza samaki mitaani.
“Mimi nitasoma mpaka niwe rubani, napenda sana kuendesha ndege. Nikiwa rubani nitakupakia wewe, mama na Sanifu”,
wote wakaangua vicheko! Hii ni baada ya Gadau kumhakikishia baba yake kwamba lazima amlipe fadhira za kumsomesha kwa shida na taabu. Kipindi hicho, Gadau alikuwa na miaka saba tu akiwa ameanza darasa la kwanza katika shule ya msingi Saja. Siku zote wanafunzi wa darasa la kwanza walikuwa wanaingia darasani asubuhi na kutoka saa nne. Hivyo kwa wakati huo Gadau alikuwa ameshamaliza kusoma na karejea nyumbani kwao. Pia huo ulikuwa ni wakati mwafaka ambao mara nyingi baba yake Gadau, mzee Tesha alikuwa akirejea kutoka bwawani.

Baada ya kifungua kinywa, Gadau alipanda baiskeli yake na kuelekea bwawani. Hakika siku hiyo ilikuwa njema sana kwake kwa sababu alibahatika kunasa samaki wengi sana kwenye mitego yake. Mitego hii ilikuwa inafahamika kwa jina la migono. Migono ni mitego inayosukwa kwa asili kwa kutumia vijiti vyembamba vinavyokuwa vinachongwa kutokana na mianzi. Kamba za miombo hutumiwa kwa ustadi mkubwa kusuka mitego hii ya asili.
Akiwa bwawani, Gadau alianza kupitia mgono mmoja baada ya mwingine na alikuwa anatega migono hamsini kila siku. Aidha njia yake ya uvuvi haikuwa ngumu sana kama wavuvi wengine ambao hulazimika kwenda katikati ya maji na kutandaza nyavu au kutupia ndoana ili kuwanasa samaki kutokana na ukweli kwamba wavuvi wa kutumia nyavu na ndoana hulazimika kulala majini! Hali hii ilikuwa nitofauti kwa Gadau ambaye yeye alilazimi kusuka migono mingi na alikuwa akiweka chambo ndani yake na kisha anaifunga majini.
Migono ni mitego ya samaki ya asili ambayo husukwa kiustadi sana na kutengeneza kitu kama pakacha. Pakacha hili huwekwa tundu kama mlango ambalo linawawezesha samaki kuingia ndani ya mtego. Ili samaki wasiweze kutoka mara waingiapo mtegoni, lile tundu la kuingilia husukwa kiasi kwamba inakuwa ni vigumu kutoka kwa sababu huwa kunakuwa na vijiti vyembamba vilivyochongoka vinavyomchoma samaki akitaka kutoka. Hivyo ukitaka kuwatoa samaki walionaswa, alilazimika kufumua migono yake upande wa chini na kuwamimina wale samaki kwenye ndoo kisha aliufuma upya na kutia chambo tena tayari kwa kutega upya!
Siku hiyo Gadau alipata samaki wengi sana wapato mia sita na themanini na mbili. Alirudi nyumbani kwa furaha kubwa sana kwani mara zote ilikuwa akipata samaki wengi basi ni mia mbili au pungufu ya hapo. Alipofika alikuta tayari wateja wake wamekuja kulangua kambale aliokuwa amewavua.
“Heee! Leo umepata samaki wengi sana”,
alisikika bibi Mulwisa akistaajabia wingi wa kambale aliokuwa amewavua Gadau.
“Leo Mungu kazidi kanibariki nimepata samaki wengi sana, mtawamaliza hawa wote kweli?”,
Gadau alihoji.
“Lazima tuwamalize, samaki ndio nyama pekee tunayoitegemea hapa kijijni, wenye ng’ombe wao hawawachinji mpaka wawe na kimeta!”,
bibi Kidenya alisisitiza. Kila mtu aliangua kicheko. Kina mama hawa walikuwa wakilangua samaki wengi kutoka kwa Gadau na kisha kuwakaanga au kuwakausha ili wasiharibike. Walikuwa wakiwauza kwa bei kubwa zaidi siku ya gulio na mnada lililokuwa linafanyika mara moja kwa mwezi huko manadani.
Mnadani ni pahala palipokuwa panafanyika mnada wa ng’ombe kila mwezi sambamba na gulio. Cha kushangaza eneo hili halikupewa jina jingine zaidi ya mnadani. Hiki ni kitongoji kidogo kilichopo katika kijiji cha saja. Saja ilikuwa na vitongoji vikubwa vitatu, kitongoji cha Mnadani, Makondo na Saja Kati. Kwa hiyo ninapokuwa nazungumzia Saja kama kijiji huwa namaanisha hivyo vitongoji vitatu.
Siku ya mnada, watu wengi walijumuika mnadani wakitokea zaidi ya vijiji saba vilivyokuwa vinakizunguka kijiji cha Saja. Pamoja na kuwa kijiji, pia Saja ilikuwa ni makao makuu ya kata. Kwa maana hiyo Saja ilikuwa ni kata yenye vijiji vya Uhenga, Ikulimambo, Idenyimembe, Igomba, Itengelo, Igenge na Isimike. Bila shaka utakubaliana nami kwamba siku ya mnada watu wengi sana walijumuika pamoja ili kujipatia mahitaji yao mbali mbali. Kina bibi Kidenya walilazimika kuwakusanya samaki wengi na kuwakausha ili wawauze siku ya mnada kwa bei ambayo iliwanufaisha kiasi japo kuwa walikuwa wakiwauza baadhi ya samaki hao kila siku kilabuni. Kilabuni kuliuzwa pombe za kienyeji maarufu kama ulanzi, komoni na kangara. Kutokana na sheria za kijiji cha Saja kilabu kilikuwa kinafunguliwa kuanzia saa kumi jioni. Ilikuwa ni kosa la jinai kwa mtu yeyote kuuza pombe kabla ya saa kumi hii ilitokana na ukweli kwamba serikali ya kijiji ilikuwa imejiwekea mikakati ya kupambana na umasikini na kuhakikisha wanakijiji wake wanafanya kazi ili kujipatia maendeleo.
Kila mwanakijiji alikuwa anaheshimu sana sheria hii na ilikuwa ukikamatwa umelewa saa za kazi yaani kabla ya saa kumi jioni, ilikuwa ni lazima uwekwe mahabusu ya kijji kwa siku tatu na umtaje aliyekuuzia pombe nyakati hizo za asubuhi ili na yeye apewe adhabu. Wanawake wengi walikuwa wanakumbwa na adhabu hii maana wapishi wa pombe na wauzaji wengi katika kijiji cha Saja walikuwa ni wanawake.
“Mimi nilidhani nitapumzika kwa siku tatu au zaidi maana nimepata samaki wengi sana lakini nashangaa naona mnawamaliza wote”,
Gadau alihoji kwa kejeli!
“Au unataka tukuachie ukae nao siku tatu?”,
huku anacheka, Bibi Mulwisa alijibu.
“Lahasha! Kwanza nilipowavua hawa samaki nikawa najiuliza kama nitapata wateja! Nashukuru Mungu mmewashambulia kama mpira wa kona”,
Gadau alihimiza.
“Utupe ofa leo, sisi ni wateja wako wa uhakika!”
Bibi Kidenya alipenyeza ombi.
“Najua umuhimu wenu maana mmekuwa wateja wazuri sana kwangu. Nitakuwa nawapa ofa mara moja kwa mwezi lakini ofa hii itaanza mwezi ujao”,
wote wakaangua vicheko mara baada ya Gadau kutangaza ofa ambayo walikuwa wanaitilia shaka.
“Ina maana hamniamini?”
“Tunakuamini sana, usije ukatukimbia tu mwezi ujao ukifika”,
bibi Mulwisa alisisitiza!
Ilipotimu milango ya saa kumi jioni, Gadau alivaa viatu vyake vya mazoezi na kuelekea uwanjani. Gadau hakuwa mlevi wa pombe ya aina yoyote ile hivyo muda wa jioni aliutumia pia kucheza mpira na vijana wenzake ambao walikuwa hawanywi pombe.
Aidha katika nyakati hizi za jioni watu wengi walikuwa wanakusanyika kilabuni wakinywa ulanzi, kangara, togwa na komoni huku wakitikisa vichwa vyao taratibu kutokana na mirindimo laini ya muziki uliokuwa unapigwa kilabuni hapo. Walevi wengi walikuwa wanapenda nyimbo za Pamela Nkuta. Hivyo kila kona ya kilabu ilisikika milindimo ya nyimbo za mwanadada huyo kutoka kwa ‘Madiba’!
Itaendelea kesho………
**********
