- Aweka Kipachiko Kwenye Ukurasa wa Mark Zuckerberg.
- Facebooka Yakana Kumlipa, Yadai Kakiuka Taratibu.
- Dunia Yalalama Ikishinikiza Alipwe!
Kama wewe ni mdukuzi na umegundua mwanya wa kuishambulia Facebook, una nafasi ya kuwasilisha ripoti yako kupitia mpango wa kampuni hiyo ya wadukuzi salama(white hat hackers) kwa kutoa taarifa na kupata tuzo. Lakini utafanyaje kama umegundua tatizo na ukatoa taarifa lakini timu ya Facebook ikakupuuza?
Mdukuzi wa Kipalestina alichukua hatua isiyoshauriwa ya kupakia kipachiko katika ukuta wa mwanzilishi wa Facebook Mark Zuckerberg, ili kumjulisha hatari ya taarifa aliyokuwa anaiwasilisha lakini akapuuzwa. Khalil Shreateh, mdukuzi wa Kipalestina, aligundua kwamba kulikuwa na njia ya kudukua faragha ya mtu katika Facebook na kuweza kupakia kitu chochote katika akaunti ya mtu hata kama mwenye akaunti hiyo ya facebook si rafiki yako.
Khalil alianza kuripoti mazingira ya facebook na namna mtu anavyoweza kudukua akaunti kupitia barua pepe kwa mpango wa kawaida uliowekwa na facebook wa kutoa taarifa za udukuzi. Lakini timu ya wadukuzi salama wa facebook ilishindwa kutambua mazingira magumu katika ripoti yake, hii ni kulingana na maelezo ya Khalil katika blog yake.
Kabla ya kuripoti, Shreateh alifanya jaribio, jaribio lililofanikiwa kiufasaha kwa kupakia kipachiko juu ya ukuta wa Sara Goodin, mwanafunzi mwenza wa Zuckerberg wa zamani wa chuo.
Khalil aliweka pia kiungo (link) cha ukurasa wa Sara Goodin kwa bahati mbaya mfanyakazi wa Facebook wa usalama wa mitandao aliyeipokea barua pepe ya Khalil aliyefahamika kwa jina moja Emrakul hakutambua tatizo licha ya kumtambua Sara. Hakuweza kuona kipachiko cha Khalil kwenye ukuta wa Sara kwa sababu hakuwa na urafiki na Sara.
Katika kuonyesha msisitizo wa tatizo alilokuwa ameligundua, Khalil alimwambia Emrakul kwamba anaweza pia kupakia kipachiko chochote kwenye ukurasa wa Mark Zuckerberg kama angetaka na akaonya kwamba hatafanya hivyo kwa sababu anaheshimu faragha za watu, hii ilikuwa ni barua pepe ya pili ya Khalil ambayo nayo pia ilipuuzwa.
Kwa mara nyingine tena Khalil Shreateh alituma ripoti nyingine rasmi kwa Emrakul ikionyesha tatizo lakini Emrakul alijibu, “Samahani, hilo sio tatizo” Khalil akajibu, “ok, hii ina maana sio tatizo, sina namna nyingine tena nitaripoti hiki kitu kwa Mark mwenyewe huko huko Facebook.” Na kweli Khalil akafanya hivyo!
Kitendo hicho kilimshtua mfanyakazi mwingine wa Facebook, Ola Okelola ambaye alitupia maoni kwenye kipachiko cha Khalil kwenye ukurasa wa Mark akitaka maelezo zaidi. Baada ya maelezo mafupi akaunti ya Khalil ilifungiwa kwa muda kwa sababu za kiusalama.
“Kwa bahati mbaya ripoti yako katika mfumo wetu wa udukuzi haikuwa na taarifa za kiufundi za kutosha ili ituwezeshe kuchukua hatua juu yake,” Yoshua aliandika. “Hatuwezi kujibu ripoti ambayo haina maelezo ya kutosha kutufanya kulishughulikia suala hilo”, Aliongeza. “kwa bahati mbaya hatutakulipa kwa hatari hii kwa sababu matendo yako yamekiuka Masharti yetu ya Huduma ya kuripoti udukuzi ili ulipwe.”, alisisitiza Yoshua.
Kwa kupakia kipachiko kwenye ukurasa wa Zuckerberg, Shreateh pia alikiuka sera na masharti ya Facebook yanayomtaka mdukuzi yeyote anazuiwa kuonyesha tatizo hadharani aliloligundua kwa kuonyesha tatizo hilo kwenye kurasa za watumiaji wengine wa facebook bila idhini yao.
Aidha jambo lililozua mjadala ni kauli ya Facebook ya kusema haitamlipa Khalil Shreateh kwa sababu alikiuka taratibu za kuwasilisha matatizo. Kumekuwana mijadala mikubwa kulaani kitendo hicho cha Facebook kwani ushahidi unaonyesha wazi kuwa Khalil Shreateh alijitahidi kwa kila hali kuwasilisha uvumbuzi wake huo bila mafanikio. Jambo alilolifanya ni kubwa sana na angeweza kutumia ujuzi huo kuwaathiri watumiaji wengine wa Facebook lakini bado Khalil Shreateh hakufanya hivyo na Facebook wameshindwa kutambua nia yake njema na kukana kumlipa.
Hata hivyo Facebook walitangaza Alhamisi hii kwamba tatizo alilokuwa ameligundua Khalil Shreateh limeshadhibitiwa. Kumekuwepo kampeni ya kushinikiza Facebook imlipe Khalil Shreateh.
Je, kwa mtazamo wako, Khalil Shreateh anastahili kulipwa? Funguka!
**********
