Mtunzi: Baraka Oscar
Baruapepe: info@vunjambavu.com
Majira ya saa kumi na mbili jioni, makundi yote yaliyokuwa yametawanyika maporini kumsaka Gadau yalirejea mikono mitupu na kukuta taarifa ya kuhuzunisha kutokana na kifo cha Magembe. Huu ni moja ya misiba iliyovuta hisia za watu wengi sana katika kijiji cha Saja. Harakati za mazishi zilifanywa na watu walijitolea kwa moyo mmoja kushiriki katika shughuli zote za mazishi kwa hali na mali. Kijiji kilihamia nyumbani kwa marehemu mzee Lugoya kuhani msiba wa kijana hodari na mchapa kazi aliyefariki akiwa na umri wa miaka ishirini na sita tu. Ratiba ya mazishi ilipangwa na Magembe alitarajiwa kuzikwa siku iliyofuatia katika makaburi ya kanisa la Lutherani.
Mapambazuko yalipowadia, waombolezaji walijiinua kutoka kwenye mikeka na vigoda walivyokuwa wamevilalia ili wajiandae kwa shughuli ya mazishi iliyokuwa ikiwakabiri mbele yao. Ilikuwa ni desturi ya wanakijiji kusitisha shughuli za maendeleo mara zote msiba ilipokuwa inatokea. Kengele ya kwanza iligongwa saa kumi na mbili na nusu alfajiri ili waombolezaji wakachimbe kaburi kwa ajiri ya kumhifadhi marehemu Magembe. Huu ni utaratibu uliokuwa umezoeleka kabisa kijijini kwani kila ulipotokea msiba watu walijidamka asubuhi na mapema kwenda kuchimba kaburi kwa ajili ya maziko. Kazi hii ilifanywa na vijana wa kiume pekee ambao wanaaminika kuwa na damu changa na wenye nguvu zaidi ya kuchimba chini kwa kimo cha futi sita.
Ilipotimia saa tatu kasorobo asubuhi siku ya Ijumaa, kaburi lenye urafu wa futi sita lilikuwa limechimbwa tayari kwa mazishi. Vijana wote walirejea msibani kupata kifungua kinywa huku wakisubiri taratibu nyingine za mazishi. Taratibu hizo zilitegemea vikao vya wanafamilia na ndugu wa karibu wa marehemu. Muda mchache baadae ratiba ya mazishi ilitolewa na Magembe alitakiwa kuzikwa saa nane mchana katika viwanja vya makaburi ya kanisa la Lutherani.
Umati mkubwa wa wanakijiji ulifurika katika kanisa na hakika kulikosekana viti vya kutosha jambo lililowalazimu baadhi ya waombolezaji kukaa nje ya kanisa.
“Masikini! Kijana huyu kweli kapata watu wengi wa kumzika”
“Hakuna ambaye hajaguswa na msiba huu, nafikiri hakuna mtu aliyebakia nyumbani leo!”
Walisikika waombolezaji wawili wakisemezana maneno hayo huku kukiwa kumetawala vilio vya kina mama kila kona ya kanisa!
Ibada ya mazishi ilifanyika kwa amani na utulivu japo kulikuwa na hekaheka nyingi kutokana na mguso mkubwa wa msiba ule kijamii. Baada ya kuuaga mwili wa marehemu kwa kutoa heshima za mwisho, majira ya saa kumi na moja jioni, msafara wa waombolezaji ulielekea makaburini tayari kwa mazishi. Mazishi yalikamilika salama salimini na waombolezaji wengi walirejea makwao huku baadhi yao wakirejea nyumbani kwa marehemu kwa ajili ya kuwafariji wafiwa.
Mzee Kiswaga alikuwa ni mmoja wa waombolezaji waliokuja kulala matanga nyumbani kwa marehemu. Alijikaza kufanya hivyo japokuwa alikuwa anasikia maneno mengi yakisemwa semwa sana kuhusiana na mfululizo wa matukio ambayo yalisababisha msiba huo mzito wa Magembe. Kila mtu alikuwa anaamini kwa namna moja au nyingine mzee Kiswaga alikuwa anahusika kama msababishaji wa tukio hilo. Ni kweli nafsi yake ilimsuta sana na alijutia kitendo chake cha kumshambulia Gadau japo kuwa hakuwa na uwezo wa kubadili kile kilichokuwa kimetokea.
Siku tatu zilipita, matanga yalianuliwa kila mtu alirejea kwake na shughuli za maendeleo zikaanza kurejea katika hali yake ya kawaida. Ni dhahiri misiba huumiza wengi sana lakini kuna msemo usemao ‘wanadamu tumeumbwa kusahau!’ Taratibu wanakijiji walianza kusahau uchungu na huzuni waliyokuwa wameipata kutokana na msiba wa kipenzi chao Magembe.
Wiki moja baadaye, mwenyekiti wa kijiji aliitisha mkutano wa hadhara wa dharura ili wanakijiji waweze kujadiliana hatima ya kile kilichokuwa kimetokea. Huu ni moja ya mikutano ambayo ilihudhuriwa na wanakijiji wengi sana. Kila mtu alikuwa na shauku ya kutaka kujua kile ambacho kingezungumzwa katika mkutano huo!
Lutengano, mwenyekiti wa kijiji cha Saja alifungua mkutano huo mara baada ya kukaribishwa na katibu mtendaji wa kijiji Bwana Tawi,
“Leo tumekusanyika hapa, tuna ajenda kubwa mbili!”
Lutengano alipenyeza ujumbe wa awali kabla hajaanza kudadavua ajenda moja baada ya nyingine. Wanakijiji walikuwa wametulia wakimsikiliza kwa umakini mkubwa sana.
“Kwanza ni kile kitendo cha kutoweka ndugu yetu Gadau katika mazingira tata na pili ni lile lilotokea wiki moja iliyopita la kumpoteza kipenzi chetu Magembe”
Baada ya kumeza funda la mate, mwenyekiti aliendelea,
“Mpaka sasa hatuna taarifa yoyote kuhusu Gadau, au kuna mwenye taarifa zake?”,
mwenyekiti alishirikisha umma. Hata hivyo hakuna mtu aliyejitokeza kutoa taarifa za Gadau. Kitendo hicho kilimpa fursa mwenyekiti kuendelee kutoa hoja zake.
“Kamati ya kijiji imekaa na kuamua kusitisha zoezi hili la kumtafuta Gadau lakini kama ulivyo utaratibu ni lazima tuafikiane katika mkutano wa kijiji! Nia ni njema lakini tumejikuta tukitengeneza tatizo kubwa zaidi la kumpoteza mpendwa mwenzetu. ”
Hapa mwenyekiti alikuwa anamaanisha kifo kilichomkuta Magembe na kuiachia familia yake na wanakijiji kwa ujumla majonzi makubwa yasiyo na kifani. Wananchi walichangia hoja mbalimbali kulingana na tukio hilo. Wapo waliotaka zoezi lisitishwe na pia kulikuwa na wanakijiji waliotaka zoezi la kumsaka Gadau liendelee.
“Maisha yetu yamekuwa magumu ghafla, nani asiyejua hapa kwamba Gadau alilisha familia zetu? Nani asiyejua hapa kwamba biashara zetu zilitegemea kazi ya Gadau? Suala la kusitisha zoezi mimi siafiki”,
Bibi Mulwisa alihoji kwa ukali huku akisisitiza kutokubaliana na usitishwaji wa zoezi la kumtafuta Gadau.
“Nataka tujue moja kama yuko hai au laa! Maana biashara zetu zimetuumbua sasa!”
Mlanguzi huyo maarufu wa samaki alitilia mkazo kuonyesha ni jinsi gani biashara yake imeathirika kutokana na kitendo cha Gadau kutoweka. Mambo mengi sana yakijadiliwa na hatimaye mwenyekiti wa kijiji aliamua kura zipigwe ili wengi wapewe haki yao.
Hatimaye kura zilipigwa na ukawadia wakati wa kusoma matokeo ya kura hizo. Wanakijiji walitulia kimya ili kujua ni kundi lipi limeshinda!
“Matokeo yamepatikana na huu ni uamzi wenu wanakijiji wa kijiji cha Saja”,
Lutengano aliwaweka sawa wanakijiji ili awasomee matokeo ya kura.
“Jumla ya kura zote zilizopigwa ni mia mbili na thelathini na saba, kura nne zimeharibika! Kura mia moja na tatu zimesema zoezi liendelee na kura mia moja na thelathini zimesema zoezi lisitishwe”
Mwenyekiti alivuta funda moja la mate na kushusha pumzi kisha akaendelea,
“Hivyo uamzi wa wengi uheshimiwe,wote kwa pamoja tumeafikiana kusitisha zoezi la kumtafuta Gadau!”
Baada ya matokeo hayo iliibuka minong’ono ya chini chini isiyo na ukomo jambo lililomlazimu mwenyekiti awafungue midomo wanakijiji kwa kuruhusu kama kuna mwenye dukuduku au swali.
“Naona kuna jambo linasemwasemwa uvunguni, ni vizuri kama kuna mtu ana neno akalisema hapa kuliko aliseme pembeni baada ya mkutano huu. Kuna mwenye neno?Naona mkono pale, karibu Lusajo!”
Lusajo alipewa fursa ya kutoa dukuduku alilokuwa nalo na ghafla minong’ono ikakoma na kila mtu akawa anataka kusikia kijana huyu angezungumza jambo gani.
“Asante sana mwenyekiti,kuna jambo moja silielewi, kutokana na kile ambacho kimetokea mimi naona mzee Kiswaga ni sababu ya yote haya. Mbona binti wa mzee Mgurunde alipewa mimba na hatukuona mzee huyu akikata mtu kwa panga wala mundu. Waliyamaliza kiutu uzima na sasa wale vijana ni mke na mume.”
“Pendekezo lako ni nini?”
“Mzee huyu awajibishwe na ailipe fidia familia ya mama Magembe”,
Umati wa watu ukapaza sauti,
“Kweliiiiii…!”
“Alipe fainiiii”
Sauti kubwa ya wanakijiji ilipazwa wakitaka mzee Kiswaga alipe faini kwa kusababisha mkasa. Wapo ambao hawakuafikiana na hili lakini wengi waliafiki jambo hili.
Mwenyekiti wa kijiji akalazimika kumaliza utata huo kwa kutoa msimamo wake. Alisisitiza kuwa wazo hilo si baya ila kamati ya ulinzi na usalama ya kijiji italijadili hilo.
“Naomba mtupe muda kwa hilo kwani hii ni hoja nzito sana na mpya; lazima kamati ikae na kulijadili. Ikipata majibu basi tutawaeleza, kwa leo mkutano wetu umefikia tamati”,
Mwenyekiti alihitimisha mkutano na watu wote wakarejea kwenye kaya zao. Kila mtu alijaribu kuzungumza kwa mtazamo wake na matarajio yake kuhusiana na hoja iliyokuwa imetolewa mwisho na Lusajo! Kwa bahati mbaya au nzuri mzee Kiswaga hakuhudhuria mkutano huo wa hadhara. Hii ilitokana na ukweli kuwa alikuwa anajua ni ajenda gani zingekuwa zikijadiliwa katika mkutano huo wa dharura. Hata hivyo tayari kulikuwa na uvumi ambao ulikuwa ukizagaa kijijini ukimshutumu kuwa yeye ndiye aliyekuwa chanzo cha mikasa yote ambayo ilikuwa imejitokeza.
Itaendelea……………………..
**********
