Nani Mwendawazimu?
Hii kweli ni sauti ya mwendawazimu, nimeamua kupayuka kama mwendawazimu kwa sababu najua hakuna atakayenisikia. Kuna mambo yanaudhi sana na ukisema utaambiwa hufatilii mambo mhimu na dunia inavyoednda. Kinachoudhi ni kile kitendo cha kufanyana wendawazimu hali najijua mimi si mwendawazimu na nina akili timamu.
Taifa letu si masikini nafikiri vichwa vyetu ni masikini wa ubongo, havina ubongo wa kutosha ndio maana wengine tukiongea tunaonekana wendawazimu. Ndio, tunaonekana wendawazimu, kuna wakati huwa najiuliza hivi akili zangu hazinitoshi mimi mwenyewe aua na za wengine haziwatoshi? Nashukuru leo nimejua wengi wetu tu wendawazimu na hakika hazitutoshi! Ni kawaida ya mijitu fulani ikikaa Dodoma huku inasinzia ikiulizwa,
“mnataka kula tena?”
Inajibu
“ndiyooooooooooooooooo!”
Inaweza ikawa ni lugha ya kuudhi ila hii mijitu imetuudhi sana na tumekuwa wendawazimu vya kutosha. Ndio, tumekuwa wendawazimu vya kutosha. Kuna jambo ambalo limenikera sana na wendawazimu wangu ni hili la kodi ya kadi ya simu kwa mwezi. Kwanza kinachoniuma sana mimi nina kadi zangu 5; vodacom, tigo, airtel, zantel na ttcl (simu la mezani)! Yote hii ni kujaribu kutafuta unafuu wa kuwasiliana kwa sababu nilichogundua ni lazima niwasiliane.
Kwa bahati mbaya hii mijitu imegundua ni lazima nitawasiliana tu, ikaamua kucheza na akili yangu. Hii tozo ya 1,000/= kwa mwezi kwa kila kadi si wazo baya lakini utata unakuja pale tunapokuwa na mifumo mibovu ya kulinda pesa za umma kama Tanzania. Sina tatizo kabisa na kodi hii lakini nina tatizo na kule pesa hizi zinakoenda. Nitakupa mfano mdogo, halimshauri ya Kibaha ilikuwa inaendesha zoezi la kukusanya tozo ya leseni kwa kila bodaboda inayobeba abiria kupitia Sumatra. Mifumo iliyotumika ni kandamizi pasipo kuchanganua bodaboda zina gharama gani na biashara yake ni imara kiasi gani. Kwanza hakuna biashara mbaya kama ya bodaboda kwani kila mtu anakuibia kuanzia dereva mpaka wewe mwenyewe unajiibia. Yamekuwa yakitumika makampuni ya kiwizi wizi kama Yono Auction kukamata bodaboda na kutoa matozo makubwa sana kama faini vitu vinavyoumiza sana watu.
Unajua hii mijitu haijui sisi wendawazimu tushapagawa sana kimaisha hivyo kila mtu anajaribu kufurukuta kutatua shida zake kimya kimya pasipo kumwambia mwenzake. Kuna mwendawazimu mmoja aliyaona haya siku nyingi na watu wanampuuza tu wakimwona mwendawazimu sana,
“…Serikali corrupt haikusanyi kodi, itabakia kukimbizana na vijitu vidogodogo mabarabarani na kuacha mijitu hailipi kodi…”
Kwa Nini Nilipe Kodi?
Serikali ina wajibu wa kutoa huduma kama za ulinzi na usalama, elimu, afya na nyinginezo zinazofanana na hizo. Kwa bahati mbaya serikali yetu haifanyi biashara hivyo inategemea kodi ili itoe huduma hizo. Kwa kifupi naweza kusema hizo huduma nazilipia kwa kodi kabla sijazitumia au wakati nazitumia huu ndio wendawazimu wangu unavyonituma.
Manji akiugua malaria na bibi yangu akiugua Malaria kule Idunda, wote watahitaji tiba ya malaria. Kwa hiyo jambo la msingi hapo ni tiba japo uuguzaji utatofautiana sana. Inawezekana mtu asielewe kwamba hata ukiwekwa Ikulu ukalazwa pale unaumwa malaria, hutapona kwa sababu umelazwa vitanda vya Ikulu lahasha! Utapona kwa sababu umetibiwa malaria hivyo sina neno kabisa na kodi kama inarudi kutumika kutoa huduma za jamii pasipo kujali natoa kiasi gani.
Kinachonikera nalipa kodi lakini bado umeme bei kali, maji hayashikiki, vyakula ndio usiseme, nauli za mabasi ni kubwa kuliko za baadhi ya ndege, huko hospitali pamekuwa ni sehemu ya kupata ushauri na vipimo tiba kanunue mwenyewe, shule zetu wendawazimu wameziita za kata hazina la maana. Nauliza kwa nini nillipe kodi? Naona ni bora nisilipe kodi kusudi niyamudu hayo magharama yote yanayoniandama!
Sasa wakati natafakari hayo yote, unanifanya mwendawazimu tena kwa kunitaka nisiwasiliane kabisa na watu ili nipate dili hata za kunipa vijisenti tano tano vyangu. Puuuh! Lazima nikukabe roho msimu huu, ndio hapa sasa umechemka!
Kwa Nini Sitaki Kulipa?
Pasipo kujali ni nani alileta wazo hili, mimi namwona mwendawazimu. Ameshindwa kabisa kukusanya kodi kwenye migodi yote hii tuliyonayo, vivutio vya asili, biashara za makampuni makubwa, bandari zetu, reli zetu anataka kuokoteza visenti kwenye kadi zetu za simu! Puuuuuh! huyu ndio mwendawazimu, kinachonipa wasiwasi zaidi mfumo wa kukusanya mapato na kuyadhibiti kwetu sisi ni mbovu sana hapa Tanzania. Watu wametoa mabilioni wameyapeleka Uswisi yanakaa tu huko wakisahau kabisa kuna siku watakufa! Hawa ni wendawazimu wakubwa, ni bora wangetuibia halafu wakatupa sandakalawe humu humu kwa kuwekeza ili tugawane umasikini wetu!
Chenji ya rada iko wapi? Mabilioni ya EPA yako wapi? Na je, mabilioni ya JK yako wapi? Yanafanya nini? yamemnufaisha nani? Tumwulize nani maswali haya? Sidhani kama nakosea kusema haya. Narudia tena sina tatizo na wazo la kukusanya kodi ya kadi za simu ila nina tatizo na mfumo wa kiwiziwizi wa kufuja pesa za umma. Kwa sasa siko tayari na kama mbwai mbwai tu! Wakianza kukata nitafuteni kwa anwani hii hapa.
Saja Shule Ya Msingi, S.L.P. 1023, Makambako, Njombe – Tanzania!
**********

Thats good,but watch out watakurukia wenye hisa kubwa za nchi.