Ni majuma kadhaa sasa yamepita tangu mjadala mzito uzuke miongoni mwa Watanzania wanaotumia simu za mikononi mara baada ya bunge la Tanzania kupitisha kodi ya kadi za simu. Kodi hiyo ya kiasi cha shilingi za kitanzania elfu moja itatozwa kila mwezi kwa mtumiaji wa simu ambaye anamiliki kadi ya simu.
Hatua hii imefikiwa kwa kile ambacho kinadaiwa ni kuongeza mapato ya serikali kwa ajili ya maendeleo ya Taifa. Lakini kwa mara ya kwanza huenda kodi hii ikakataliwa na Watanzania kwani wanasiasa na wananchi kwa ujumla wamekuwa wakifanya mijadala mikali kwa lengo la kuipinga kodi hii ambayo imeanza kutumika Julai Mosi mwaka huu!
Aidha aina hii ya kodi haitofautiani sana na tozo za bodaboda ambazo zilikuwa zikitozwa na SUMATRA kwa wenye pikipiki zinazofanya biashara ya kupakia abiria ambayo ilileta usumbufu sana kwa wananchi wa kipato cha chini ambao wanajaribu kujikwamua kiuchumi kutokana na hali mbaya ya kimaisha. Kumekuwa na mijadala mikali katika mitandao ya kijamii ambayo inapinga kwa nguvu zote ulipaji wa kodi hii ya kadi za simu!
Zitto Kabwe, mbunge wa CHADEMA ameonyesha kuendeleza mjadala huo katika mtandao wa facebook huku akiungwa mkono na wafuasi wake wengi zaidi. pia mbunge huyu amekuwa akitoa njia mbadala za serikali kuongeza mapato ambazo zimeachwa ikiwemo misamaha mikubwa ya kodi, posho za wabunge na mawaziri wanapokaa katika vikao na nyinginezo nyingi. Mapambano haya yamekuwa yakiongozwa pia na mbunge kijana John Mnyika wa CHADEMA naye akikerwa na uwekwaji wa kodi hii.
Kuna taarifa kwamba Watanzania wameanza kusaini kitabu kupinga tozo ya kodi hiyo na iwapo Watanzania wengi wataipinga basi huenda kodi hii ikakwaa kisiki kutoka kwa watoa ridhaa ya madaraka yaani wananchi! Vyombo mbalimbali vimekuwa vikiripoti taarifa hii ikiwemo BBC Swahili na vinginevyo. Ifuatayo ni sehemu ya ripoti ya BBC iliyoripotiwa siku za hivi karibuni.
Shukrani: BBC Swahili
