Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CDM) kimerejesha kata nne zilizokuwa zinagombaniwa katika uchaguzi mdogo mjini Arusha siku ya Jumapili na hivyo kuendeleza ubabe wake dhidi ya chama tawala katika mji huo ambao ni lango kuu la maeneo ya utalii nchini. Ushindi huo wa ngurumo umekuja baada ya waliokuwa wanachama na madiwani wa CDM kuvuliwa uanachama baada ya kufanya uasi na kusababisha viti vinne vya udiwani kuwa wazi kitu kilichosababisha kuitishwa kwa uchaguzi mdogo. Uchaguzi wa kata hizi nne umefanyika zikiwa zimepita karibu wiki kadhaa tangu kufanyika kwa chaguzi nyingine ndogo ambapo katika kata za Arusha uchaguzi wake uliahirishwa kufuatia mlipuko wa mabomu katika mkutano wa kampeni wa CDM ambapo watu watatu waliuawa na wengine zaidi ya sabini kujeruhiwa.
Matokeo Ya Uchaguzi Mdogo Wa Madiwani – Arusha |
||||
| Na. | KATA | CHADEMA | CCM | CUF |
| 1 | Elerai | 1715 | 1239 | 213 |
| 2 | Kaloleni | 1019 | 389 | 169 |
| 3 | Kimandulu | 2665 | 1169 | – |
| 4 | Themi | 678 | 326 | 313 |
Kimsingi, CDM imeshinda kwa zaidi ya asilimia 61 ya jumla ya kura halali zilizopigwa; ni ushindi wa radi! CCM wametumiwa ujumbe mzito wa kuwafanya watafakari kama wapo watu wenye kutafakari.
Kilichofanyika Arusha ni kichapo cha mwaka; ni uthibitisho kuwa kukataliwa kifikra hutangulia kukataliwa kivitendo na hapa vitendo ninamaanisha kura. Kwamba, kabla ya watu hawajabadilisha kura zao ni lazima wabadilishe fikra zao kwanza; wananchi wa Arusha walishabadilisha fikra zao kuhusu Chama cha Mapinduzi tangu 1995 walipomchagua Makongoro Nyerere wa NCCR-Mageuzi na toka wakati ule mahusiano yao na CCM hayajawa ya kawaida. Na siyo Arusha mjini tu ni katika Arusha ambapo tumeona upinzani ukizama hadi vijijini – Karatu, Mbulu, Arumeru Mashariki na Arusha Mjini kote ni wabunge wa upinzani na wote ni wa CDM. Ni mkoa wenye wabunge wengi wa CDM kuliko mkoa mwingine na mahali ambapo kama isingekuwa mizengwe basi Halmashauri karibu tatu za miji mbalimbali zingekuwa chini ya CDM. Kwa matokeo haya na kama hakutakuwa na mizengwe ya CCM Meya ajaye wa Arusha atatoka CDM.
Wananchi wa Arusha hawakujali sana ahadi, vitisho, kejeli na vioja vya watawala; na ni wazi kabisa kuwa hawakujali zaidi milipuko ya mabomu na unyanyasaji uliopitiliza wa vyombo vya dola. Ni Arusha ambapo viongozi karibu wote wa CDM wamejikuta wakidhalilishwa, kufunguliwa mashtaka na kunyanyaswa na wale wenye madaraka ya kutawala. Kuanzia Mbowe hadi Slaa, Bi. Mushumbusi hadi Lema wote wamepata kibano chao mjini Arusha. Katika mazingira ya kawaida watu wanaweza kufikiria kuwa ili wawe “salama” na ili mambo yao yafanyike kwa “utulivu” si bora wachague CCM tu? Ni rahisi kabisa kuamini kuwa kwa kuchagua CCM Arusha ingekuwa imetulia na watu wake wana amani. Kwanini pamoja na ahadi hiyo ya nchi ya “maziwa na asali” wananchi wa Arusha bado wameikataa CCM?
Jibu linaweza kuwa ni gumu kidogo na lina mambo mengi. Kwa kuanzia tunaweza kusema kuwa wananchi wa Arusha wamekataa kupiga magoti mbele ya wanaowadhulumu na mbele ya watawala walioshindwa. Mwanadamu akinyanyasika sana kuna mahali anafika ambapo katika kukataa kwake kunyanyasika zaidi anaamua kukataa – kwa kiburi – kupiga magoti. Historia imejaa watu wa namna hiyo; watu ambao kwa kujitambua utu wao na thamani yao hawakuwa tayari kujisalimisha mbele ya watawala ili wapate amani ya uongo.
Lakini kubwa zaidi tunaweza kusema kuwa watu wa Arusha tofauti kulinganisha na mji kama wa Dar wengi wao ni wafanyabiashara na wanajitegemea wao wenyewe kwa maisha yao. Ni watu ambao wanashughuli mbalimbali ambazo hazitegemei ajira ya serikalini. Jiji kama la Dar kwa mfano lipo kundi kubwa sana la kipato cha kati ambalo linategemea maisha yake serikalini. Kundi hili kwa kiasi kikubwa ni kikwazo sana cha mabadiliko Jijini Dar kwani hawa ni watu ambao hata kama wanachukia yanayoendelea ni vigumu kuchagua upinzani kwa sababu hawaoni kama maslahi yao yatalindwa. Arusha na miji mingi ya pembezoni wako huru zaidi kuchagua bila ya kujali athari zozote kwenye ajira zao. Pamoja na kuchagua upinzani wananchi wa Arusha wameendelea kujipatia vipato vyao na ajira zao na utulivu ambao unatarajiwa kuja baada ya kuchagua chama wanachotaka kunaweza kurejesha amani na utulivu zaidi kama serikali na Chama cha Mapinduzi havitaendelea kuleta mizengwe.
Matokeo ya awali ya uchaguzi huu yanatuma ujumbe mwingine zaidi. Kwamba, bado juhudi kubwa sana ya kukandamiza upigaji kura zinafanyika nchini na hili tumeanza kuliona tangu 2010. Katika hali ambayo haijawahi kutokea kabla ya 2010 upigaji kura ulikuwa chini ya asilimia 70 (asilimia karibu 40 hivi). Chaguzo zote kuu za nyuma yake upigaji kura ulikuwa kati ya asilimia 69 kwenda juu. Hata hivyo CCM ikitumia mbinu zinazoeleweka sana – vitisho, kukatisha tamaa, kufanya upinzani uonekane ni shetani, n.k imefanikiwa sana kukatisha tamaa ya kupiga kura hasa kwa wazee na kina mama. Hivyo, upinzani umekuwa ukitegemea kura za vijana zaidi kuliko za makundi mengine. Kundi hili la vijana sasa ndio ngome kuu ya upinzani nchini; na hawa ni vijana hasa ambao ama walipiga kura kwa mara ya kwanza 2010 au ndio wanapiga kura kwa mara ya kwanza sasa.
Lakini kuna kitu kingine ambacho naamini ni kweli zaidi kuliko hivi vingine na nilikidokeza katika posti yangu ya Facebook mapema leo; CCM inazidi kukataliwa na ahadi zake hazivutii tena kama zamani, vitisho vyake haviogopeshi na utukufu wake hautukuzwi tena. Ni wazi kabisa kuwa kukiwa na Tume huru, na mfumo mzuri wa uchaguzi CCM itapata shida sana kushinda na badala yake inahitaji sana kutegemea dola (polisi, wakuu wa wilaya, wakuu wa mikoa n.k) kuweza kushinda. Hili ndilo tatizo kubwa sana; CCM ili kujirejeshea uhalali siyo tu ikubali kushindwa baada ya uchaguzi bali ichague njia yenye kuonesha kuwa uchaguzi ni huru na wahaki na hakuna njia nzuri ya kufanya hivyo kama kuhakikisha uhuru wa vyombo na uhuru wa sheria ya uchaguzi.
Hivyo, walichokifanya watu wa Arusha ni kuamua kuicharaza CCM kwenye sanduku la kura; kwani ni hapo tu ndipo sauti za raia zinaweza kusikika vizuri. Hofu ile ya kuwa CCM wataiba kura ni hofu ambayo imezuia watu wengi kupiga kura kwa sababu wanajiambia kuwa ‘CCM itashinda tu’ na matokeo yake hawaendi kupiga kura. Watu wa Arusha wamejua nguvu ya kura yao na wanajua sauti yao ni kura yao. Hawawezi kushindana na polisi na usalama wa taifa; hawawezi kushindana na Mkuu wa Mkoa na IGP; lakini wanajua sehemu pekee ambapo wana uwezo wa kushindana ni kwenye kupiga kura. Na hivyo wamejitokeza kupiga kura. Ni kama walipewa fimbo na kuambiwa waende wakawachape CCM na kuwachapa wamewachapa. Haikujalisha nani aliipigia kampeni CCM au jinsi gani CCM ilibebwa, mwisho wa siku (siku ya uchaguzi) uamuzi wa mwisho ni wa mtu mmoja mmoja; watu ambao walishafanya uamuzi wao kwenye fikra wakaenda kuuthibitisha kama kutia sahihi kwenye sanduku la kura.
Wananchi wetu wengi wakielewa nguvu hii kuu waliyonayo na nguvu ambayo inafanya demokrasia inoge watatambua kuwa iwe kwa mbinde au kwa upinde wataenda kupiga kura. Kwamba, haijalishi mabomu, polisi, kejeli au vitisho, ikifika wakati wa kupiga kura wataenda kupiga kura na kusema kile ambacho hawawezi kukisema kwa maneno.
CCM imekataliwa. Na huu ni mwendelezo tu wa yale ambayo tumeyaona tangu 2010. Kazi kubwa ni kuwashawishi mamilioni ya wananchi wengine ambao kwa woga au kutokujua wanafikiri kuwa CCM inatakiwa kutawala milele.
Arusha wamesema hapana na wamerudia kusema hivyo tena na tena. CCM iheshimu uamuzi wa wananchi wa Arusha na iache mizengwe kwani haikisaidii chama kupendwa zaidi; CCM iangalie watu wake wanaoifanyia kampeni kama ni watu ambao wanastahili kuendelea na hilo kwani zaidi ya kuwafanya wapoteze kura, watu hao wamezidi kuifanya CCM ionekane ni kituko na kejeli na kudharaulika. CCM ikiendelea na watu wale wale na mbinu zile zile wapinzani hawana la kufanya isipokuwa kuendelea kucharaza watu bakora ya kura; ndio utamu wa demokrasia.
Hata hivyo yote ni sehemu ya demokrasia; Katibu Mwenezi wa CCM Nape Nnauye amesema vizuri kuelezea hili katika mtandao wa JamiiForums baada ya kipigo cha Arusha “Kuna watu wameuliza sana juu ya matokeo ya uchaguzi Arusha, but jibu la harakaharaka katika kila uchaguzi kuna kushinda na kushindwa, na mshindani wa kweli lazima ajiandae kwa yote maana asiyekubali kushindwa si mshindani.(kama mabo yote yamekwenda sawa)”.
Shukrani: Mwanakijiji
